Ticker

6/recent/ticker-posts

Athari Ya Kukosa Sheria Rafiki Ya Vyombo Vya Habari

 


Na Thuwaiba Habibu, Zanzibar

Ni zaidi ya miongo miwili sasa wanahabari wamekuwa wakililia  sheria ambazo ndani yake vimo vifungu vinavyokandamiza uhuru wa kupata na kutoa habari zirekebishwe.

Wakati jamii ikishuhudia  sheria nyingi za nchi zikibadilishwa mara kwa mara, nyingine muda mchache tu baada ya kupitishwa na Baraza la Wawakilishi, lakini hizi zinazogusa habari zimekuwa na safari ya zaidi ya miaka 20 na mwanga wa kupatikana ufumbuzi haujachomoza.

 Kwa miaka hiyo yote waandishi wa habari wa Visiwani Zanzibar wamekuwa wakililia marekebisho ya sheria za habari ili angalau wapate nafasi ya kufanya kazi kwa usalama kama wenzao wa sekta nyingine.

Kilio cha waandishi wa habari wa Zanzibar kutaka sheria za habari zifanyiwe marekebisho kinatokana na misukosuko wanayokumbana nayo kila siku wakati wakiwa kazini.

Ikiwa ni pamoja na kuporwa vifaa vya kazi kama kamera, simu, chombo cha kunasia sauti, vitabu vyao wanavyoandikia habari, kalamu na hata fedha na wakati mwingine kubugudhiwa  kwa kupigwa au kufunguliwa mashitaka.

Mwandishi wa habari na Mjumbe wa (ZAMECO)  Jabir  Idirisa anasema  yeye ni miongoni mwa waandishi waliokumbana na mashtaka kwa kufungulia kesi ambayo aliishi nayo kwa muda wa miaka 6  kuanzia  Januari 2016 hadi Septemba 2021 akituhumiwa kufanya uchochezi kwa kutimiza wajibu wake wa kutoa taarifa ambayo ni haki ya wananchi.

"Lazima kuwepo kwa sheria rafiki ambayo inaondoa hali ya kudhibiti sana  vyombo vya habari na itakuwa imewapa uhuru waandishi wa kufanya kazi zao."

Anasema waandishi wanapitia shida kubwa japo kuwa wao ndio wachagizaji wa maendeleo nchini.

Mwandishi wa habari Amrat Kombo anasema kuwapo kwa sheria isiyo rafiki yenye vifungu vinavyokwaza uhuru wa habari  kunawatia hofu waandishi juu ya usalama wa maisha yao.

Ameelezea sheria mbili kuu zinazohusu masuala ya habari; ambazo ni Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu, Na. 5 ya mwaka 1988 kama ilivyorekebishwa na Sheria Na. 8 ya mwaka 1997; na pia Sheria ya Tume ya Utangazaji ya mwaka 1997 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2010; akisema kuwa hizo bado ni dhaifu katika kulinda uhuru wa habari visiwani hapa.

Kutokana na sheria hizo, waandishi  wamekuwa wakipitia changamoto kadhaa kwani kila kitu kuhusu uhuru wa habari kimedhibitiwa.

Haya yanafanyika wakati Tanzania ikiwa imeridhia mikataba mingi ya kikanda na kimataifa inayosisitiza umuhimu wa uhuru wa habari na wa kujieleza.

Mikataba hii ni pamioja na ule wa Kimataifa wa Haki za Binadamu (UDHR) wa 1948 ambao umebainisha umuhimu wa kuwapo kwa uhuru wa kujieleza kwa kila binadamu.

Vile vile mkataba  haki za kiraia na kisiasa  wa 1966 (ICCPR) ambao unaeleza kuwa kama italazimika kuwapo vikwazo ni mambo mawili tu; nayo ni kwa ajili ya kuheshimu faragha ya mtu na usalama wake.

Mikataba yote imeeleza wazi wazi kuwa kila mtu ana haki ya kujieleza, kupokea maoni na kusambaza maoni yake bila ya vikwazo.

Afisa Programu  wa  Tamwa – Znz, Zaina Mzee aliwasihi wanahabari kutokata tamaa na kuendelea kudai haki yao ya kuwa na uhuru wa kukusanya na kusambaza habari kwa usalama.

"Endeleeni kufanya uchechemuzi ili tuweze kupata sheria mpya na rafiki ya habari ambayo itatufanya tuweze kufanya kazi zetu vizuri."

Mwana habari Mkongwe, Hawra Shamte alisema lazima kuwe na msisitizo wa upatikanaji wa sheria mpya za habari  ili uhuru wa habari na haki ya kujieleza ipatikane na kuchangia maendeleo.

Pia amesema  upo umuhimu wa kuwepo  mashirikiano na watunzi wa sera na serikali kufufua sekta hii ili kuwapa nafasi wandishi kuandika vizuri habari na kuelimisha umma juu ya masuala mbali mbali .

 

Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ), Dkt. Mzuri Issa alieleza mchakato wa mabadiliko ya sheria za habari umekuwapo kwa miaka mingi lakini bado sheria hizo ambazo nyingi ni za muda mrefu zimekwama kurekebishwa na kukosesha uhuru kwa vyombo vya habari, waandishi na hata wanajamii, kwani uhuru wa kujieleza, uhuru wa maoni na uhuru wa kusambaza taarifa ni wa kila mmoja wetu.

“Sisi wengine tangu tuko waandishi chipukizi tunazungumzia kupata hizi sheria mpya za habari, tangu 2008 kwa kweli ni muda mrefu, tunahitaji kusimamia jambo hili kwa umoja wetu na hatimaye tupate sheria mpya.

Post a Comment

0 Comments