Ticker

6/recent/ticker-posts

Utekelezaji Wa Mikataba Ya Kuwainua Wanawake Imeachwa Nyuma Zanzibar

 


NA AMRAT KOMBO, ZANZIBAR: 

Nchi nyingi zimeridhia mikataba na matamko ya usawa wa kijinsia, uwezeshaji wanawake kwenye uongozi na nafasi za maamuzi kama ilivyoainishwa katika Tamko la Haki za Binadamu la mwaka 1948.

Zanzibar nayo ikiwa sehemu ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo imesaini mikataba ya kikanda na kimataifa, lakini safari ya utekelezaji wake ni ndefu na hii inaonekana katika shehia, wadi, majimbo, taifa kutokana na kutokuwepo fursa sawa katika kugombea uongozi.

Mikataba iliyosainiwa na hali halisi ya uongozi kwa wanawake Zanzibar ni wazi kuwa mikataba ya kikanda na kimataifa haijazingatiwa vyema hapa nchini katika kutoa fursa sawa ya uongozi kati ya wanaume na wanawake.

TAKWIMU ZA UCHAGUZI 2020.

Katika uchaguzi mkuu wa 2020 watu walioteuliwa na vyama kugombea nafasi ya ubunge kwa upande wa Zanzibar wanaume 257 na walioshinda 46, wanawake walikua 81 na walioshinda wanne.Walioteuliwa kugombea nafasi ya wawakilishi Zanzibar  wanaume 190 na walioshinda 42 ambapo wanawake walikuwa 61 na walioshinda ni 8 na wanaume walioteuliwa na vyama kugombea udiwani 276 na walioshinda 85 ambapo wanawake walikua 74 na walioshinda ni 25.

MIKATABA NA ITIFAKI INASEMAJE?

Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) ambayo mkataba wake ulitiwa saini mwaka 2008 inaeleza kutaka kuondoa utafauti na kuwatenga wanawake katika nyanja mbalimbali za maendeleo na kusaidia kuwepo usawa wa kijinsia katika nchi wanachama na kufikia asilimia 50/50 kwenye maamuzi, serikali na taasisi binafsi.

Mkataba mwengine wa kimataifa wa (CEDAW) wa 1979 ambao unapinga aina zote za udhalilishaji na kusisitiza ushiriki wa wanawake katika siasa na maisha ya kijamii.

Kwa mfano itifaki ya Jumuiya ya Maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) mkataba wake wa kikanda uliotiwa saini mwaka 2008 na nchi wanachama wake ikiwemo Tanzania, wenye vifungu 43 unaelekeza nchi hizo kuzingatia suala la haki na usawa kati ya wanaume na wanawake katika suala la uongozi.

Kifungu cha nambari 12 kinasisitiza ushiriki sawa wanawake na wanaume kufikia asilimia 50/50 kwenye Nyanja za maamuzi, serikalini na taasisi binafsi.Katika Itifaki ya Maputo ambayo makubaliano yake yalifanyika tarehe 11, Julai 2003 nchini Msumbiji, kipengele nambari 9 kinahimiza ushiriki sawa wa wanawake na wanaume katika siasa na vyombo vya kutoa maamuzi. Aidha jukwaa la Mpango wa Utekelezaji wa Beijing mwaka 1995 kifungu nambari 7 kinataka ushiriki katika vyombo vya maamuzi kwa kuzingatia uwiano wa kijinsia kwenye ngazi zote za uongozi.

KATIBA YA ZANZIBAR

Katiba ya Zanzibar ya 1984, imeweka wazi kuwa kila Mzanzibari anayo haki na uhuru wa kushiriki kwa ukamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo  yanayohusu taifa lake na katika marekebisho ya 2010 imeeleza kutakuwa na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi (BLW) asilimia 40 wa wajumbe kwa kila jinsia.

DIRA NA SERA ZA ZANZIBAR

Dira ya Zanzibar ya 2050 imeelezea jinsi gani masuala ya usawa wa jinsia juu ya kuondoa unyanyasaji na kuimarisha mifumo ya uwezeshaji wanawake, ikiwa pamoja na kuinua na kutoa nafasi za uongozi kwa wanawake.

Vile vile imelenga kuongeza fursa na kuwawezesha katika vyombo vya kutoa maamuzi na kwenye shughuli za uchumi, kijamii, siasa, ngazi za utawala na huduma za sheria.

Sera ya jinsia inaeleza ushiriki wa wanawake katika vyombo vya utoaji maamuzi katika ngazi zote ni mdogo hivyo serikali kwa kushirikiana na wadau wengine imeahidi kufanya juhudi kuona makundi yote na yaliyopembezoni yanapata fursa hiyo.

MTAZAMO WA VYAMA VYA SIASA

Asha Abdallah mkaazi wa mahonda ambae pia mwakilishi wa jimbo hilo.na kujuzwa kuwa bado  utekelezaji wa mikataba kuwainua wanawake  imeachwa nyuma ,kutokana na ushiriki mdogo wa wanawake katika kushika nafasi mbalimbali za uongozi ,kwa mfano wawakilishi wanawake mwaka 2015 ilikuwa 7 na mwaka 2020 wako 8 hii inaonesha dhahiri kuwa mikataba imeachwa nyuma.

Naibu Mkurugenzi kutoka ADC, Mtumwa Faiz Sadik, amesema ili kuzipatia ufumbuzi changamoto wanazopitia wanawake ni lazima kuwepo mipango mizuri ya kutekeleza mikataba na maazimio ya kimataifa.”Mikataba haitekelezwi ipasavyo na kuchangia kutofikiwa usawa kati ya wanawake na wanaume katika kuwania uongozi licha ya wanawake kujipanga na kuhamasika kugombea katika uchaguzi mkuu wa hivi karibuni.

Kiongozi wa ACT Wazalendo, Juma Duni Haji, amesema chama hicho kinafuata sheria na mikataba iliyoridhiwa na kusistiza hakina mfumo dume na kutoa mfano wa sekretieti ambayo ni chombo kikubwa kuwekewa uwiano wa wajumbe, wanaume 10 na wanawake 10.

KINACHOKWAMISHA 

Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) upande wa Zanzibar, Tunu Juma Kondo, amesema ipo haja ya kuzingatia mikataba ya usawa kwenye uongozi kati ya wanawake na wanaume na kusisitiza kwamba hivi sasa wanawake wameelimika, wanafahamu mambo ya siasa, uchumi na maendeleo, ni vyema mikataba itekelezwe.”Mfano mzuri ni wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, ambaye anaifanya kazi yake kwa bidii kuimudu nyadhifa hioo kuu nchini kwa uadilifu mkubwa, kutokana na kutouwepo sheria inayotaka kuwepo fursa zenye hadhi sawa kwa wanawake na wanaume kunaifanya nchi kutotekeleza kwa ufanisi baadhi ya mikataba iliyoridhia inayohusu usawa katika uongozi.”Amesema Tunu

NINI KIFANYIKE.

Mwanaharakati maarufu wa haki za wanawake Daktari Ananilea Nkya ameishauri serikali na wadau wa masuala ya sheria kuona umuhimu wa utekelezaji mikataba iliyosainiwa.” Naomba kuwashauri serikali pamoja na wadau mbalimbali wa masuala ya sheria kuzingatia sheria zilizowekwa kwenye mikataba na wasiipe kisogo kwani utekelezaji wa mikataba hiyo itakuwa njia ya kuwainua wanawake katika siasa.vilevile nawashauri wanawake wenzangu kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa mwaka 2025 ili kufikia azma ya kuanzishwa mikataba ya kitaifa na kimataifa.”Amesema Ananilea

Kwa upande wake mwanaharakati wa Chama Cha Habari Wanawake Tanzania – Tamwa Zanzibar mkurugenzi wa chama hicho Dkt Mzuri Issa amesema umefika wakati kuondoa vikwazo vinavyokwamisha mikataba hiyo.”Ni vyema vyama vya siasa kuwekwa sheria rafiki zitakazotoa muongozo wa matamko hayo ili kuzingatiwa mikataba hayo ipasavyo.  Karne hii ya sasa inawapasa viongozi wa vyama vya siasa kubadilisha katiba zao kuendana na mikataba iliyoridhiwa ili kufikia uwiano wa 50/50 kwenye siasa na serikali kwa ujumla".Ameongezea Dkt Mzuri

Post a Comment

0 Comments